Tamasha Chato kuhamasisha utalii wa ndani

KUTOKANA na tafiti mbalimbali zilizofanyika Tanzania, utalii ni sekta ambayo ina nguvu ya
uzalendo, amani na utajiri ambao ni zawadi na karama kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kuijalia nchi ya Tanzania kuwa na neema ya vivutio vingi vya utalii tofauti na nchi nyingine ulimwenguni.
Tanzania ni ya pili kwa vivutio duniani baada ya Brazil. Hivyo, kutokana na umuhimu wa
sekta hiyo, Halmashauri ya Wilaya ya Chato mkoani Geita imekuja na tamasha maalumu la Chato Utalii Festival linalotarajia kuanza kesho Jumapili Novemba 26 mpaka Desemba 3, mwaka huu.
Halmashauri ya Wilaya ya Chato mkoani Geita imehamasika kuwa na wazo la kuandaa tamasha hilo katika kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii, utamaduni wa Mtanzania na kuhamasisha utalii wa ndani kuanzia ngazi ya kaya hadi kwenye wakala wengine wa malezi ikiwemo shuleni, vyuoni.
Akizungumza na gazeti la HabariLEO katika mahojiano maalumu, Mkuu wa Wilaya ya Chato, Deusdedith Katwale anaongeza kuwa tamasha hilo linalenga kukuza na kuinua uchumi wa nchi na watu wake kupitia fursa mbalimbali zilizopo kupitia sanaa, maliasili, vivutio vya Taifa na kutangaza umuhimu wa amani na rasilimali hii adimu ya vivutio mbalimbali vya utalii na kuonesha kwa vitendo uzalendo kwa rasilimali ilizojaliwa Wilaya ya Chato.
Anasema ndani ya tamasha la utalii la Chato kutakuwa na makongamano ya uwekezaji katika uvuvi, utalii pamoja na kilimo. Amesema Hifadhi ya Taifa ya Rubondo inakadiriwa kuingiza watalii 3,000 kwa mwaka kutoka nje ya nchi.
Anasema wao kama halmashauri wana mpango kwa kuhakikisha kwa mwaka 2027 hifadhi hiyo inaingiza watalii 50,000 mpaka 100,000 kwa mwaka. Naye Mhifadhi mwandamizi wa
Hifadhi ya Taifa Burigi-Chato, Ombeni Hingi amesema watatumia tamasha la Chato Utalii Festival kama sehemu mojawapo ya kuhamasisha utalii.
Hingi amesema lengo kuu la tamasha hilo kutangaza fursa mbalimbali za utalii katika Wilaya ya Chato na fedha itakayopatikana itasaidia katika kukabiliana na changamoto ya uhaba wa madawati 29,000 katika wilaya hiyo.
Amesema Hifadhi ya Taifa ya Burigi- Chato ni moja kati ya hifadhi kubwa ambapo hifadhi hiyo ni ya nne kwa ukubwa kati ya hifadhi 21. Amesema watalii watapata fursa ya kuona wanyama watano wakubwa ambao baadhi ni tembo, nyati, simba na chui.
Amesema uongozi wa hifadhi yao upo katika mpango mwaka huu wa kurejesha faru weupe katika hifadhi hiyo. Amesema pia tamasha hilo litakutanisha mechi maalumu kati ya mashabiki wa timu za Simba na Yanga katika Uwanja wa Magufuli wilayani Chato Mkoa wa Geita, lenye lengo la kutangaza vivutio vya utalii.
Akielezea zaidi kuhusu mchezo huo wa watani utapigwa Jumatano ijayo mwaka huu huku michezo mingine ikiwa ni mbio za baiskeli kilometa 80 (Chato –Katete), mashindano ya mitumbwi kilometa 8 (Kisiwa cha Rubondo –Mwerani), mapambano ya ngumi na riadha kilometa 5, kilometa 10 na kilometa 21 ambazo washiriki watajiandikisha kwa Sh 35,000.
“Mechi hii itaratibiwa na viongozi wa juu wa hizi timu mashabiki kutoka sehemu mbalimbali wataunda timu na kucheza ni mchezo wa furaha na burudani, tunategemea itakuwa fursa
nzuri kwa viongozi wao kufurahia na mashabiki kwa sababu wasemaji Ali Kamwe na Ahmed Ally wameshiriki mwanzo wa mchakato huu na waliahidi kuwepo,” amesema Hingi.
Naye Ofisa Mhifadhi wa Taifa Kisiwa cha Rubondo, Themistocles Bitta amesema siku ya ufunguzi wa tamasha hilo kutakuwa na mashindano ya mbio za baiskeli kutoka eneo la
Chato kuelekea eneo la Katete.
Anasema Novemba 27 kutakuwa na mashindano ya mbio za mitumbwi kutoka Rubondo kwenda Mwelani. Anasema Desemba 2 kutakuwa na mashindano ya mbio za marathon za
kilomita 5, 10 na 21. Anasema usajili wa mbio hizo ni shilingi 35,000 kwa washiriki.
Bitta anasema Desemba 3 kutakuwa na tamasha la Nyamachoma kwa ajili ya kufunga tamasha la Chato Utalii Festival. Anasema katika tamasha hilo kutakuwa na burudani za wasanii kama vile Zuchu na Saida Karoli.
Anawaomba Watanzania kushiriki kwa wingi tamasha hilo, kutembelea hifadhi, kujifunza fursa mbalimbali na kuchangia Pato la Taifa.
“Tamasha hili ni ndoto ya wana Chato kuifanya kuwa ya kimataifa, Chato iliyochangamka na iwe kitovu cha utalii pia tuifanye kuwa eneo ambalo lina maendeleo watu wanataka kuiona Chato inabadilika. Kisiwa cha Rubondo tuna utalii wa ziwani, utalii wa uvuvi, sokwe, kutembea kwa miguu na kuangalia vivutio ukiwa ndani ya gari,” anasema.
Naye Mkurugenzi wa kampuni ya usafirishaji ya Lau Tours, Laurent Laurian, amesema kampuni yake itatoa usafiri kwa washiriki wote wa tamasha hilo watakaoshiriki katika tamasha.
Amesema washiriki watanufaika na gharama za kutembelea hifadhi za Burigi-Chato na Rubondo kwa gharama za shilingi 45,000 safari ya kutwa na Sh 75,000 kulala hifadhini.
Chato Utalii Festival upo chini ya udhamini wa benki ya NMB, Halmashauri ya Wilaya ya Chato, pori butchery, Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Lau tours and safaris pamoja na DSTV.