Africa

Cameroon yavunja laana ikitwaa ubingwa Wafcon 2026

RABAT: CAMEROON imeandika historia mpya katika soka la wanawake Afrika baada ya kutwaa taji la kwanza la Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON), ikiwafunga Malawi mabao 3-0 katika fainali iliyochezwa Rabat, Morocco.

Timu hiyo maarufu kwa jina la Indomitable Lionesses walitawala mchezo huo tangu mwanzo na walimaliza kazi mapema baada ya kufunga mabao yote matatu katika kipindi cha kwanza, huku Malawi iliyokuwa ikicheza fainali kwa mara ya kwanza ikishindwa kupata jibu.

Marie Ngah Manga ndiye aliyeanzisha sherehe hizo kwa kuifungia Cameroon bao la kwanza, kabla Naomi Eto kuongeza la pili kwa mkwaju uliomwacha mlinda mlango wa Malawi akiwa hana nafasi ya kuzuia.

Ngah Manga alikamilisha siku yake kwa kufunga bao la tatu na la pili kwake katika mchezo huo, akifikisha mabao yake matano katika michuano hiyo na kumaliza akiwa miongoni mwa wafungaji bora wa WAFCON 2026.

Ushindi huo umevunja pia historia ya Cameroon ya kufika fainali na kuishia mikono mitupu, baada ya awali kupoteza fainali tatu, ikiwamo ile ya mwaka 2016 iliyoangukia kwa Nigeria kwa bao 1-0.

Kwa upande mwingine, Malawi imeondoka Morocco ikiwa na heshima baada ya kufika fainali katika ushiriki wake wa kwanza wa WAFCON, safari iliyochangiwa kwa kiasi kikubwa na kiwango bora cha mshambuliaji wake Temwa Chawinga.

Chawinga alimaliza michuano hiyo akiwa na mabao matano na pasi mbili za mabao, akiongoza kwa jumla ya michango saba ya mabao. Idadi hiyo ilimfanya kuwa mchezaji aliyekuwa na ushawishi mkubwa zaidi katika mabao miongoni mwa wafungaji bora wa michuano hiyo.

Chawinga alifunga mabao mawili katika ushindi wa Malawi wa 3-2 dhidi ya Nigeria katika mchezo wa ufunguzi, kabla ya kuendelea kufunga dhidi ya Misri, Ghana na Algeria.

Zambia pia ilipata mwakilishi katika orodha ya wafungaji bora kupitia nahodha wake Barbra Banda, aliyemaliza akiwa na mabao matano na asisti moja. Banda alianza michuano kwa kishindo baada ya kufunga mabao manne katika ushindi wa Zambia wa 6-0 dhidi ya Misri.

Kwa jumla, Chawinga, Banda na Ngah Manga walimaliza WAFCON 2026 wakiwa kileleni mwa chati ya wafungaji, kila mmoja akiwa na mabao matano.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button