
DAR ES SALAAM: BONDIA wa Ngumi za kulipwa nchini, Ibrahim Mafia atapanda ulingoni kesho katika pambano lisilo la ubingwa la raundi 10, uzito wa kati (Kg 50) dhidi ya Prasitsak Phaprom kutoka Thailand.
Pambano hilo kuu litasindikizwa na pambano la mtanzania Said Chino (kilo 61) akitarajia kuzichapa dhidi ya Simpiwe Vityeka wa Afrika Kusini katika ukumbi wa City Centre uliopo Magomeni Sokoni jijini Dar es Salaam.
Mabondia wengine ambao watanogesha pambano Kuu ni kati ya Richard Mtangi ambaye atacheza dhidi ya Magambo Christopher huku Salmin Kasim akipambana na Abert Kimario kutoka Kenya.
Wengine ni Yohana Mchanja dhidi ya Joseph Akai, Ramadhan Ramadhan na Guy Tshimanga wa Jamhuri ya Kidemkrasia ya Congo (DRC) na Ramadhan Kimoko dhidi Harvey Mkacha kutoka Malawi.
Akizungumza na Spotileo baada ya kupima uzito, Bondia Said Chino amesema yupo fiti kuelekea katika pambano la kesho.
“Mashabiki zangu wategemee mambo mazuri kutoka kwangu, kwani nimejipanga vizuri na kuwapa furaha mashabiki zangu na watanzania kwa ujumla, “amesema Chino.
Naye Mkurugenzi msaidizi wa Mafia Boxing Promotion, Ally Zayumba amesema pambano hilo la kimataifa litakuwa na mapambano 15 huku nane kati ya hayo yakiwa ya kimataifa.
“Wadau wa ngumi leo watapata burudani nzuri kwa sababu kila bondia anayecheza yupo vizuri, nawaomba wajitojeze kwa wingi, tiketi zinauzwa mlangoni, “amesema Zayumba.