Hanks: Disney inaweza kutumia AI kuihuisha sauti ya muigizaji kwenye filamu yake

NEW YORK: Muigizaji mkongwe wa Hollywood, Tom Hanks, amesema anaamini kampuni ya Disney inaweza kutumia teknolojia ya akili bandia (AI) kuendelea kutumia sauti ya mhusika Woody katika filamu zijazo za ‘Toy Story’ hata pale ambapo yeye hatakuwa tayari kurejea kuigiza.
Hanks, ambaye ameipa sauti tabia ya Woody tangu filamu ya kwanza ya Toy Story mwaka 1995, alisema maendeleo ya teknolojia ya AI yamefikia kiwango kinachoweza kuiga sauti ya mtu kwa uhalisia mkubwa. Alisema jambo hilo linaweza kuifanya studio kuendeleza mhusika huyo maarufu bila kulazimika kumrekodi tena kila wakati.
Muigizaji huyo alieleza kuwa matumizi ya AI katika tasnia ya filamu yanaendelea kuibua mjadala mkubwa kuhusu haki za wasanii na umiliki wa sauti pamoja na sura zao. Alisisitiza kuwa teknolojia hiyo inaweza kuwa na manufaa makubwa, lakini ni muhimu kuwepo kwa ridhaa ya mhusika na ulinzi wa haki za wasanii ili kuzuia matumizi yasiyoidhinishwa.
Kauli ya Hanks imekuja wakati Disney na Pixar wakiendelea na maandalizi ya filamu mpya ya Toy Story, huku mashabiki wakisubiri kuona iwapo Woody na wahusika wengine maarufu watarejea.
Mjadala kuhusu matumizi ya AI katika filamu unazidi kushika kasi Hollywood, huku wadau wakitaka teknolojia hiyo itumike kwa kuzingatia maadili na haki za wabunifu.




