Dabi ya Kariakoo takwimu zinaibeba Yanga, Simba presha tupu

ZANZIBAR:KIPUTE cha watani wa jadi kati ya Yanga na Simba kinatarajiwa kupigwa Jumapili, Machi 01, 2026, kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar kuanzia saa 2:15 usiku.
Mchezo huo unakuja katika kipindi ambacho Yanga wanaingia wakiwa na rekodi bora dhidi ya watani wao, baada ya kushinda mechi sita mfululizo za mwisho za Dabi ya Kariakoo.
Katika michezo hiyo sita, Yanga waliibuka na ushindi wa mabao 5-1, 2-1, 1-0, 1-0, 2-0 na 1-0 dhidi ya Simba, wakionesha ubabe wa wazi katika miaka ya karibuni.
Takwimu hizo zinaweka presha kubwa kwa Simba ambao wataingia dimbani wakihitaji kuvunja mwendelezo huo na kurejesha heshima yao mbele ya mashabiki.
Waamuzi Watajwa
Kamati ya waamuzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imemtaja Nassoro Mwinchui kuwa mwamuzi wa kati katika pambano hilo, akisaidiwa na Kassim Mpanga na Hamdan Said, huku Ramadhani Kayoko akiwa mwamuzi wa akiba.

Rekodi zingali Hai
Historia ya dabi hiyo iliyoanza mwaka 1965 imebeba matukio mengi makubwa ambayo baadhi yake hayajawahi kuvunjwa hadi sasa.
Miongoni mwa rekodi hizo ni ya Abdallah Kibadeni wa Simba aliyefunga mabao matatu katika dabi ya mwaka 1977, akiwa mchezaji pekee kufunga ‘hat-trick’ katika historia ya pambano hilo.
Katika mechi hiyo, Simba waliibuka na ushindi wa mabao 6-0, huku mabao mengine yakifungwa na Jumanne Hassan aliyefunga mawili na bao moja likiwa la kujifunga la beki wa Yanga, Seleman Sanga.
Aidha, mwaka 2013 katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, Yanga waliwahi kuongoza kwa mabao 3-0 kabla ya Simba kusawazisha na kufanya matokeo kuwa 3-3 katika mchezo uliovuta hisia za mashabiki wengi.
Pia mwaka 1996 kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, timu hizo zilitoka sare ya mabao 4-4 katika moja ya mechi zenye mabao mengi zaidi katika historia ya dabi hiyo.
Dakika 90 Za Maamuzi
Licha ya rekodi na takwimu, dabi ya Kariakoo imekuwa ikijulikana kwa matokeo yasiyotabirika.
Yanga wataingia wakisaka kuendeleza ubabe wao wa hivi karibuni, huku Simba wakisaka ushindi wa kurejesha matumaini na kuvunja mwiko wa kupoteza mechi sita mfululizo. Itakuwa ni presha kwa wekundu hao ambao muda mrefu hawajaifunga Yanga.
Mashabiki sasa wanasubiri kuona nani atatabasamu baada ya dakika 90 ndani ya Amaan Complex.




