Tennis

Sabalenka amtoa Osaka, atinga robo fainali

PARIS:BINGWA namba moja duniani wa tenisi Aryna Sabalenka ameendelea kuonesha ubora wake katika michuano ya French Open baada ya kumtoa Naomi Osaka kwa ushindi wa seti 7-5, 6-3 na kutinga hatua ya robo fainali ya mashindano hayo yanayoendelea jijini Paris, Ufaransa.

Sabalenka alipata upinzani mkali kutoka kwa Osaka katika mchezo huo wa hatua ya 16 bora uliochezwa usiku wa Juni 1, lakini alitumia uzoefu na nguvu zake za mashambulizi kugeuza mchezo na kuibuka na ushindi muhimu katika harakati zake za kutwaa taji lake la kwanza la French Open.

Osaka alianza vizuri kwa kuongoza mapema 2-0 katika seti ya kwanza, alionekana kuwa katika kiwango bora. Hata hivyo, Sabalenka alirejea kwa kasi na kusawazisha mchezo kabla ya kupata mapumziko muhimu katika mchezo wa 11 na kufunga seti hiyo kwa ushindi wa 7-5.

Katika seti ya pili, Sabalenka ameendelea kutawala kwa mashambulizi makali yaliyomuweka Osaka chini ya presha kubwa. Alifanikiwa kupata mapumziko mengine muhimu na kuongoza 4-3 kabla ya kuhitimisha seti hiyo kwa ushindi wa 6-3 na kufuzu robo fainali.

Baada ya ushindi huo, Sabalenka alimpongeza Osaka kwa kiwango alichoonesha akisema alikuwa mpinzani mgumu kutokana na mchezo wake wa kushambulia.

“Ninafurahi jinsi nilivyoweza kumrudishia presha. Pia nimefurahia namna nilivyotumikia vizuri na kwa ujumla nimecheza mchezo mzuri,” amesema Sabalenka.

Katika hatua ya robo fainali, Sabalenka atakutana na Diana Shnaider wa Urusi ambaye alimshangaza Madison Keys wa Marekani kwa ushindi wa seti 6-3, 3-6, 6-0.

Related Articles

Back to top button