Kwingineko

Kompany: Tuna kila sababu ya kujiamini

MADRID, Hispania: KOCHA wa Bayern Munich, Vincent Kompany, amesema kikosi chake kina kila sababu ya kuwa na imani kubwa baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 ugenini dhidi ya Real Madrid katika mchezo wa kwanza wa robo fainali ya UEFA Champions League.

Kompany amesema jambo muhimu kwa sasa si kulewa ushindi huo, bali ni kuhakikisha Bayern wanaendeleza kasi waliyonayo kabla ya mchezo wa marudiano utakaochezwa Aprili 15 nyumbani kwao. Amesema wanafahamu wazi kuwa Real Madrid ni timu yenye uwezo wa kufanya jambo la kipekee wakati wowote, hivyo hawataki kulegeza kamba.

Bayern kwa sasa wako kwenye kiwango bora baada ya kucheza michezo 14 mfululizo bila kupoteza katika mashindano yote, huku pia wakiendelea kuongoza mbio za kutetea ubingwa wao wa Bundesliga. Hali hiyo imeongeza matumaini ndani ya kikosi hicho cha Ujerumani kuelekea pambano la marudiano dhidi ya mabingwa hao wa Hispania.

Akizungumza baada ya ushindi huo muhimu, Kompany amesisitiza kuwa Bayern wanaiheshimu Real Madrid, lakini kwa upande mwingine wamejijengea sababu za kutosha za kujiamini kutokana na kiwango wanachoonesha uwanjani. Kwa mtazamo wake, kikosi hicho kimefanya kazi ya kutosha hadi kufikia hatua ya kuwa na ujasiri wa kutafuta matokeo makubwa dhidi ya wapinzani wakubwa kama Real.

Historia inaonesha kuwa ushindi huo ni wa maana kwa Bayern, kwani mara ya mwisho kuifunga Real Madrid jijini Madrid ilikuwa mwaka 2017, waliposhinda pia kwa mabao 2-1, ingawa baadaye walitolewa baada ya Real kufunga mabao mawili katika muda wa nyongeza na kusonga mbele.

Aidha, Bayern hawajaiondoa Real Madrid katika mfumo wa michezo miwili tangu mwaka 2012, walipofanikiwa kuitoa katika nusu fainali ya Champions League kwa mikwaju ya penalti. Rekodi hiyo inaonesha wazi kuwa kazi bado haijaisha licha ya ushindi walioupata Bernabeu.

Sasa macho yote yataelekezwa katika mchezo wa marudiano, ambapo Bayern watakuwa na lengo la kulinda ushindi wao na kukata tiketi ya kutinga nusu fainali kwa msimu wa pili mfululizo, huku Real Madrid wakisaka kufanya kile walichokizoea katika michuano hiyo kurudi kwa kishindo.

Related Articles

Back to top button