Filamu

EACLC yafungua milango wasanii wa filamu

DAR ES SALAAM: MKURUGENZI wa Kituo cha Biashara na Usafirishaji Afrika Mashariki (EACLC), Dk. Cathy Wang, amefanya mazungumzo na Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania, Dk. Gervas Kasiga, kwa lengo la kufungua fursa mpya za ushirikiano zitakazonufaisha tasnia ya filamu nchini.

Mazungumzo hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salaam, yamelenga kuimarisha mahusiano kati ya EACLC na Bodi ya Filamu Tanzania, huku yakifungua milango kwa wadau wa filamu na michezo ya kuigiza kunufaika na miundombinu ya kituo hicho kikubwa cha kibiashara.

EACLC ni kituo chenye zaidi ya maduka 2,000, kikiwa na mandhari ya kipekee pamoja na fursa mbalimbali zinazoweza kutumika katika utayarishaji wa filamu.

Akizungumza katika kikao hicho, Dk. Wang amesema kituo hicho kiko tayari kushirikiana na wanatasnia wa filamu kwa kuruhusu matumizi ya eneo hilo kama mandhari ya upigaji picha bila malipo.

Hata hivyo, amesisitiza umuhimu wa kudumisha usafi na utunzaji wa mazingira baada ya kukamilika kwa shughuli hizo.

Aidha, amewakaribisha wadau wa filamu na michezo ya kuigiza kutembelea EACLC ili kujionea fursa zilizopo na kuzitumia kujiongezea kipato.

Kwa upande wake, Dkt. Kasiga amepongeza uwekezaji mkubwa uliofanywa katika kuanzisha kituo hicho, akieleza kuwa mbali na kunufaisha wafanyabiashara, pia kinatoa nafasi kwa sekta nyingine kama tasnia ya filamu kutumia miundombinu hiyo kuongeza thamani ya kazi zao.

Aidha, ametoa wito kwa wanatasnia wa filamu nchini kufika katika kituo hicho ili kutumia fursa zilizopo kuboresha ubora na ushindani wa kazi zao.

Related Articles

Back to top button