Ligi Kuu

Mgunda: Mchezo dhidi ya JKT hautakuwa rahisi kwetu

DAR ES SALAAM:KOCHA Mkuu Juma Mgunda, amesema timu yake imejiandaa vizuri kwa mchezo unaofuata dhidi ya JKT Tanzania huku akisisitiza umuhimu wa kuwaheshimu wapinzani na kutimiza wajibu wao ndani ya uwanja.

Mgunda amesema moja ya kanuni muhimu katika soka ni kumheshimu mpinzani, hivyo Namungo itaingia uwanjani ikiwa na heshima kubwa kwa wapinzani wao, huku ikifahamu kuwa mchezo huo hautakuwa rahisi.

“Katika mpira kuna kanuni moja ya msingi ambayo ni kumheshimu mpinzani. Sisi tunamheshimu mno mpinzani wetu na tunazingatia kanuni. Ninaamini haitakuwa mechi rahisi kwa sababu tunakutana na timu ambayo nayo inahangaika kutafuta matokeo.

“Kilichopita kimepita. Kinachobaki ni kuangalia namna ya kupata matokeo katika mchezo unaofuata. Kama mwalimu, ninapaswa kuwaandaa vijana wangu kwa ajili ya mchezo huo,” amesema Mgunda.

Kocha huyo amesema anatambua umuhimu wa mchezo huo kwa pande zote mbili, akieleza kuwa kila timu itaingia uwanjani ikiwa na malengo yake na hivyo kutarajia ushindani mkubwa.

Kwa upande wa Kocha wa JKT Tanzania Ahmad Ally amesema wamejipanga kuhakikisha wanafanya vizuri nyumbani hasa baada ya kutoka kufanya vibaya katika michezo ya awali.

JKT imecheza michezo mitatu na haijashinda hata mmoja zaidi ya kuambulia sare moja na vipigo viwili.

 

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button