Ligi Kuu

Mngqithi: Hatujapata muda ila tutapambana

DAR ES SALAAM: KOCHA Mkuu wa Yanga, Manqoba Mngqithi, amesema timu yake haijapata muda wa kutosha kujiandaa kwa mchezo dhidi ya Pamba Jiji utakaochezwa kesho kwenye Uwanja wa KMC, Dar es Salaam, lakini amesisitiza kuwa lazima waingie uwanjani kupambana kusaka pointi tatu.

Mngqithi amesema ratiba imewapa muda mfupi wa maandalizi, huku akiamini hali hiyo pia inamkabili kocha wa Pamba Jiji, Francis Baraza.

“Nitakuwa muongo nikisema tumepata muda wa kutosha kujiandaa kwa mechi hii. Tumekuwa na muda mchache wa maandalizi, lakini hatuna namna; lazima tuingie uwanjani kusaka alama tatu. Najua pia Kocha Baraza naye hajapata muda wa kutosha wa kujiandaa,” amesema Mngqithi kwenye mkutano na Waandishi wa Habari Leo.

Kocha huyo amemuelezea Baraza kuwa amefanya kazi kubwa katika kujenga kikosi cha Pamba Jiji, licha ya kupoteza baadhi ya wachezaji wake muhimu waliokwenda kujiunga na timu kubwa, ikiwemo Simba.

“Kocha Baraza amefanya kazi kubwa sana katika kutengeneza timu yake. Nafahamu amepoteza baadhi ya wachezaji wake muhimu kwa vigogo kadhaa, ikiwemo Simba. Licha ya kuondoka kwa nyota wake, bado ametengeneza kikosi kizuri sana. Ana wachezaji wazuri ambao tunapaswa kuwa makini katika kuwazuia,” amesema.

Kuhusu kiungo mshambuliaji Aziz Ki, Mngqithi amesema mchezaji huyo hatakuwepo katika mchezo huo kutokana na kuchelewa kuungana na wenzake katika maandalizi ya msimu, hivyo bado hajawa tayari kwa ushindani.

Aidha, amesema mshambuliaji Clement Mzize anaendelea kuimarika na muda si mrefu atakuwa tayari kuanza kucheza.

Kwa upande wake, Kocha wa Pamba Jiji, Francis Baraza, amesema kikosi chake kimefanya maandalizi ya kutosha kwenye Uwanja wa nyasi bandia kwa ajili ya kukabiliana na Yanga, akisisitiza kuwa wataingia kwa tahadhari licha ya kuwa na dhamira ya kupata matokeo.

Baraza amesema wanaiheshimu Yanga kutokana na ubora ilionao, hivyo maandalizi yao yamelenga kuhakikisha wanakabiliana vyema na changamoto watakayokutana nayo katika mchezo huo.

Related Articles

Back to top button