Ligi Kuu

Makoma: Nimekuja kutwaa mataji

DAR ES SALAAM: KIUNGO mpya wa Azam FC, Donovan Makoma, amesema amejiunga na klabu hiyo akiwa na lengo la kutwaa mataji, akiahidi kutumia uzoefu na ubora wake kuisaidia timu hiyo kufikia malengo yake katika msimu ujao.

Makoma, raia wa Ufaransa aliyesajiliwa akitokea Birkirkara ya Malta, amesema alichokikuta ndani ya Azam FC kimempa imani kuwa amefanya uamuzi sahihi wa kuhamia Tanzania, huku akieleza kuwa hii ni mara yake ya kwanza kucheza soka barani Afrika.

“Nimeiona timu, kocha na klabu kwa ujumla. Kila kitu kiko vizuri na nina furaha kuwa hapa. Hii ni mara yangu ya kwanza kucheza Afrika na nina matumaini ya kufanya makubwa na timu,” amesema.

Kiungo huyo wa ukabaji amesema Azam FC ni klabu yenye malengo makubwa ya mafanikio, jambo lililomshawishi kujiunga nayo, akisisitiza kuwa yupo tayari kutoa kila alichonacho ili kuisaidia kushindania ubingwa.

“Nimekuja kutoa uzoefu wangu na ubora wangu wa soka. Nipo tayari kwa changamoto hii kwa sababu najua klabu inataka kushinda mataji. Nitafanya kila niwezalo kuisaidia timu na kuwafanya mashabiki wafurahi,” amesema.

Makoma mwenye umri wa miaka 27 alizaliwa Lille, Ufaransa na aliwahi kuichezea timu ya taifa ya Ufaransa chini ya miaka 16. Katika maisha yake ya soka amepitia akademi ya Lens kabla ya kuzichezea klabu mbalimbali ikiwemo Barrow na Stevenage za England, UE Santa Coloma ya Andorra, FC Cosmos Koblenz na FC Karbach za Ujerumani, kabla ya kutua Birkirkara ya Malta.

Ana uwezo wa kucheza kiungo mkabaji, kiungo wa kati na hata beki wa kati kutokana na umbile lake la mita 1.90.

 

Related Articles

Back to top button