Kwingineko

Raphina awalalamikia waamuzi

....Barca yatupwa nje

MADRID, Hispania: WINGA wa Barcelona, Raphael Dias ‘Raphinha’, amewashambulia waamuzi kufuatia timu yake kuondolewa katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na Atletico Madrid.

Barcelona ilitolewa kwa jumla ya mabao 3-2 licha ya kushinda 2-1 katika mchezo wa marudiano uliochezwa Jumanne, huku wakimaliza michezo yote miwili wakiwa na wachezaji 10 uwanjani.

Raphinha, ambaye hakushiriki michezo hiyo kutokana na majeraha, aliwashutumu waamuzi Clement Turpin na Istvan Kovacs kwa kile alichodai kuwa ni maamuzi ya upendeleo dhidi ya timu yake.

“Kwa mtazamo wangu, huu ulikuwa wizi. Sio mechi hii tu bali hata ile ya kwanza,” amesema.

Ameongeza kuwa kiwango cha uamuzi kilikuwa cha chini na baadhi ya maamuzi yalikuwa ya kushangaza, akidai kuna hofu isiyoeleweka kuhusu Barcelona kushinda.

Katika mchezo wa kwanza, beki wa Barcelona alitolewa nje kwa kadi nyekundu kufuatia mapitio ya VAR, tukio lililosababisha Atletico Madrid kupata bao kupitia Julian Alvarez.

Hali kama hiyo ilijirudia katika mchezo wa marudiano, ambapo mchezaji mwingine wa Barcelona alitolewa nje kwa kosa lililofanana, jambo lililochangia timu hiyo kushindwa kusonga mbele.

Raphinha amesisitiza kuwa makosa ya waamuzi yanaweza kutokea, lakini kurudiwa kwa makosa hayo kwa mtindo ule ule kunatia shaka na kunahitaji kuangaliwa kwa makini.

Wakati huo huo, UEFA bado haijatoa tamko rasmi kuhusu malalamiko hayo licha ya Barcelona kuwasilisha pingamizi lao.

Related Articles

Back to top button