Michezo Mingine

Kriketi yatanguliza mguu mmoja Kombe la Dunia

DAR ES SALAAM: Timu ya taifa ya Kriketi kwa vijana chini ya umri wa miaka 19 inazidi kung’ara katika michuano ya kufuzu Kombe la Dunia inayoendelea nchini Nigeria baada ya jana kushinda mchezo wa nne katika michuano hiyo dhidi ya Kenya.

Ushindi huo unaiweka timu katika nafasi nzuri ya kufuzu kwani wanahitaji kushinda mchezo mwingine ujao dhidi ya Sierra Leone hapo kesho ili kushiriki Kombe la Dunia itakayofanyika hapo baadaye Namibia na Zimbabwe.

Katika mchezo huo wa Jana Tanzania ilishinda kwa mikimbio 114/10 dhidi ya 60/10 ya Kenya. Michezo mingine ya awali iliyoshinda ni dhidi ya Nigeria, Uganda, na Namibia.

Wachezaji waliofanya vizuri na kuongoza katika mashambulizi ni Hamza Ally, Khalidy Juma na Raymond Francis.

Mchango wa Raymond ulikuwa wa maana sana, kiasi cha kumfanya ashinde tuzo ya Mchezaji Bora wa Mechi kwa mara ya pili kwenye michuano hii, akionyesha utulivu na umahirii.

Kwa ushindi huo mfululizo Tanzania inaongoza kundi hilo ila wenyewe hawataki kusherehekea hadi mwisho wa mashindano.

Chama cha Kriketi Tanzania (TCA), kimesema kinajivunia vijana hao kwa matokeo wanayopata, yanayotokana na ari, nidhamu, na kujitolea na kuwatakia kila la heri katika mchezo unaofuata.

“Hii ni kampeni iliyojengwa kwa uwekezaji, mifumo thabiti ya msaada na mipango sahihi. Miundombinu, mafunzo, na mazingira mazuri yaliyowekwa na TCA sasa yanaonyesha matunda yake katika jukwaa la kimataifa,”ilisema taarifa ya chama hicho.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button