Rybakina, Sabalenka kukutana fainali US Open

NEW YORK, Marekani: ELENA Rybakina amefuzu kwa mara ya kwanza katika historia ya kucheza fainali ya US Open baada ya kuonesha moyo wa kupambana na kumshinda mwenyeji Coco Gauff kwa seti 3-6, 6-4, 6-4.
Ushindi huo umemuweka Mkazakh huyo kwenye nafasi ya kukutana na Aryna Sabalenka katika fainali inayotarajiwa kuwa moja ya vita kubwa zaidi za tenisi mwaka huu.
Rybakina, ambaye anatarajiwa kuwa namba moja mpya duniani Jumatatu, amefanikiwa kuvunja utawala wa Sabalenka uliodumu kwa wiki 99 kileleni mwa viwango vya dunia.
Hata hivyo, kabla hajavaa taji la malkia mpya wa tenisi, atalazimika kwanza kumzuia Sabalenka kutwaa taji la US Open kwa mara ya tatu mfululizo.
Sabalenka, raia wa Belarus, aliingia fainali kwa kishindo baada ya kumtwanga Jessica Pegula kwa seti 7-5, 6-2. Baada ya kuanza kwa kusuasua na kufanya makosa kadhaa, bingwa huyo wa Grand Slam mara nne alirejea kwenye kiwango chake na kuachia mashambulizi makali yaliyomfanya Pegula ashindwe kuhimili presha.
Kwa Sabalenka, fainali hii ni zaidi ya kutetea ubingwa. Ni nafasi ya kuhitimisha utawala wake wa muda mrefu kama namba moja duniani kwa ushindi mkubwa, huku Rybakina akiwa tayari amehakikisha atachukua nafasi hiyo.
Sabalenka pia anaingia akiwa na rekodi nzuri dhidi ya mpinzani wake, baada ya kushinda mikutano 10 kati ya 17 waliokutana, ingawa Rybakina ndiye aliyemshinda katika fainali ya Australian Open mwezi Januari.
Rybakina alilazimika kutoa kila alichokuwa nacho dhidi ya Gauff, hasa baada ya kupoteza seti ya kwanza na baadaye kuvunjwa wakati akihudumia kwa ajili ya ushindi. Badala ya kuyumba, Mkazakh huyo alikusanya nguvu, akarudi kwenye mchezo na hatimaye kuufunga mdomo umati wa mashabiki wa Marekani uliokuwa ukimshangilia Gauff.
“Nilihema kwa kina na kujisemea kwamba nilipaswa kupambana na kuonyesha tenisi nzuri,” alisema Rybakina, ambaye anawania taji lake la tatu la Grand Slam baada ya kutwaa Wimbledon mwaka 2022 na Australian Open mwaka huu. Pamoja na ushindi huo, Rybakina amekiri kwamba atalazimika kuongeza kiwango chake katika fainali, hasa kwenye huduma na umakini wa kushambulia.
Fainali hiyo inavutia zaidi kwa sababu kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2013, mbegu mbili za juu katika upande wa wanawake zitakutana katika fainali ya US Open. Sabalenka pia anataka kujiunga na orodha adimu ya wanawake katika zama za Open waliofanikiwa kutwaa taji la New York mara tatu mfululizo, huku Rybakina akitafuta kuthibitisha kwamba kupanda kwake hadi kileleni mwa dunia si jambo la bahati.
Kwa rekodi yao, historia na nafasi zao katika viwango vya dunia, kila kitu kinaashiria fainali yenye presha kubwa. Sabalenka anataka kuondoka akiwa bingwa na kuendeleza utawala wake New York, wakati Rybakina anataka kuanza enzi yake mpya akiwa namba moja duniani kwa kunyanyua kombe. Jumamosi, macho ya dunia ya tenisi yatakuwa kwenye pambano hilo malkia anayeng’olewa dhidi ya mrithi anayekuja kuchukua ufalme.




