Madrid, Casablanca katika ushindani mwenyeji fainali za Kombe la Dunia 2030

RABAT, MOROCCO: Morocco imeongeza presha katika mbio za kuwania uenyeji wa Fainali ya Kombe la Dunia 2030 baada ya Rais wa Shirikisho la Soka la Morocco (RMFF), Fouzi Lekjaa, kusema kuwa fainali hiyo itachezwa katika eneo la Benslimane, karibu na Casablanca.
Kauli hiyo imetengeneza mvutano mpya katika maandalizi ya mashindano hayo, ambayo yataandaliwa kwa pamoja na Morocco, Spain na Portugal.
Lekjaa alitoa kauli hiyo Alhamisi wakati akizungumza katika hafla mjini Bouznika, Morocco. Alisema Benslimane itapata heshima ya kuandaa mchezo huo mkubwa, huku kauli yake ikionesha wazi kuwa Morocco inaamini ina nafasi kubwa ya kushinda mbio hizo. Hata hivyo, FIFA bado haijathibitisha rasmi taarifa hiyo.
Benslimane iko takribani kilomita 60 kutoka Casablanca, ambako unaendelea ujenzi wa Hassan II Stadium, uwanja mkubwa unaokadiriwa kugharimu karibu dola bilioni moja. Uwanja huo unatarajiwa kuwa na uwezo wa kuchukua watazamaji 115,000 na, ukikamilika, utakuwa miongoni mwa viwanja vikubwa zaidi vya soka duniani.
Spain nayo imeonesha nia kubwa ya kuandaa fainali hizo, jambo linalofanya ushindani kati ya mataifa hayo mawili kuwa mkali.

Rais wa Shirikisho la Soka la Spain, Rafael Louzan, alisisitiza hivi karibuni kuwa Spain inapaswa kupewa nafasi ya kuandaa mchezo huo wa mwisho wa mashindano.
Kombe la Dunia la 2030 litakuwa la kihistoria kutokana na mfumo wake wa kipekee. Kwa mara ya kwanza, mashindano hayo yatahusisha nchi sita katika mabara matatu. Argentina, Paraguay na Uruguay zitaandaa mechi za ufunguzi, huku sehemu kubwa ya mashindano ikiendelea Morocco, Spain na Portugal.
Licha ya Morocco kujitangazia matumaini ya kuandaa fainali, FIFA imesisitiza kuwa bado haijafanya uamuzi. Msemaji wa shirikisho hilo alisema uamuzi kuhusu uwanja wa fainali utafanywa baadaye. FIFA pia ilikanusha taarifa zilizodai kuwa Rais wake, Gianni Infantino, tayari alikuwa ameiahidi Morocco kuandaa fainali hizo.
Kwa Morocco, kupata fainali itakuwa mafanikio makubwa katika juhudi zake za kujenga hadhi ya taifa hilo katika soka la kimataifa. Ujenzi wa Hassan II Stadium na maandalizi ya miundombinu mingine vinaonesha matarajio makubwa ya nchi hiyo, lakini Spain bado ni mshindani mwenye nguvu katika vita hivyo.
Hadi sasa, hakuna mwenyeji rasmi wa Fainali ya Kombe la Dunia 2030 aliyetangazwa, hivyo kauli ya Lekjaa haimaanishi kuwa uamuzi tayari umefanyika.
Mashabiki wa soka duniani sasa wanasubiri FIFA itoe neno lake la mwisho kuhusu eneo litakalopata heshima ya kuandaa mchezo huo, huku Morocco na Spain zikiendelea kupigania nafasi hiyo kwa nguvu zote.




