Riyama: Mume wangu ni mdogo

DAR ES SALAAM: MSANII wa filamu nchini Tanzania, Riyama Ally, amesema hajali kauli za watu wanaomkosoa kuhusu tofauti ya umri kati yake na mume wake, akisisitiza kuwa jambo la msingi katika mahusiano ni upendo, heshima na kuelewana.
Riyama amesema baadhi ya watu wamekuwa wakisema kuwa anapendelea kuwa na wapenzi au kutoka na wanaume wadogo kwa sababu mume wake anamzidi kwa umri, jambo ambalo amesema halimsumbui kwa kuwa kila mmoja ana mtazamo wake kuhusu mapenzi.
Amesema tofauti ya umri katika mahusiano haipaswi kuwa kigezo cha kuamua kama watu wanaweza kuishi pamoja, bali kinachopaswa kupewa kipaumbele ni heshima na namna wanavyosimamia maisha yao ya pamoja.
“Wanasema mimi napenda watoto wadogo, mume wangu ni mdogo, blabla, lakini mimi kwangu naona wanazungumza wanajichoresha.
Mapenzi ni mapenzi na tumewaaminisha na tumekuwa role model wa watu wengi, mimi na mume wangu,” amesema Riyama.
Kwa upande mwingine, Riyama amesema amekuwa akiwasaidia wasanii wengi wa kike katika safari zao za kisanii, licha ya baadhi yao kutotambua au kutotaka kueleza mchango wake.
Amesema amewahi kukutana na baadhi ya wanawake waliokuwa wakipitia changamoto mbalimbali za maisha, hivyo akaamua kuwasaidia kwa kuwaunganisha na sanaa kama njia ya kujenga maisha yao.
“Nimewasaidia wasanii wengi sana, sasa hivi wana maisha na wana maisha. Nimewakuta wanapigwa danadana, wengine wakifanya shughuli ambazo hazikuwa nzuri, hivyo nikaamua kuwasaidia na kuwaingiza kwenye sanaa,” amesema.
Riyama amesisitiza kuwa anafurahia kuona baadhi ya watu aliowahi kuwasaidia wameendelea katika maisha na kujenga nafasi zao ndani ya tasnia ya burudani.
Kwa mtazamo wake, mafanikio ya msanii hayapaswi kuangaliwa pekee kwa umaarufu anaoupata, bali pia namna anavyoweza kuwasaidia wengine kupata fursa na kubadilisha maisha yao kupitia vipaji walivyonavyo.




