
ATLANTA: Kocha wa Misri Hossam Hassan amesema hatafuatilia tena mechi zilizobaki za Kombe la Dunia 2026 baada ya timu yake kuondolewa kwa maumivu katika hatua ya 16 bora.
Misri ilikuwa njiani kuandika historia baada ya kuongoza mabao 2-0 hadi dakika za mwisho, lakini ilishuhudia Argentina ikigeuza mchezo na kushinda kwa mabao 3-2 yaliyofungwa katika dakika za mwisho.
Akizungumza baada ya mchezo, Hassan amesema timu yake ilinyimwa haki kutokana na maamuzi ya waamuzi na VAR, akidai walistahili kupewa penalti huku bao lao la pili likifutwa kwa sababu ambazo hakuona zinaeleweka.
“Nitarejea nyumbani na sitaangalia tena mechi zozote za Kombe la Dunia. Kilichotokea kwetu hakikuwa cha haki. Tulistahili kupata penalti na bao letu likafutwa, sijui kwa sababu gani,” amesema Hassan.
Bao lao lilifutwa baada ya VAR kubaini kulikuwa na faulo katika mwanzo wa shambulizi. Baadaye Misri ilidai ilistahili penalti baada ya kuvutwa ndani ya eneo la hatari, lakini mwamuzi hakutoa penalti. Sekunde chache baadaye Argentina ilifunga bao la ushindi katika dakika ya 92.
Hassan amesema makosa ya wachezaji yaliyosababisha mabao yanaweza kutokea, lakini kosa kubwa zaidi lilikuwa kutopatiwa haki na wale waliokuwa na jukumu la kufanya maamuzi.
“Mimi sipendi kushindwa, lakini maumivu makubwa yanakuja pale unapohisi umeondolewa isivyo haki. Ninachoweza kuwaambia mashabiki ni wasivunjike moyo, tulifanya kila tulichoweza kuwafurahisha,” amesema.
Licha ya kuondolewa, Hassan aliwapongeza wachezaji wake kwa kupambana dhidi ya mabingwa watetezi, akisisitiza kuwa wengi wao wanacheza ligi ya ndani ya Misri huku ni wachache pekee, akiwemo na Mohamed Salah, wanaocheza soka la kulipwa barani Ulaya.
Amesema kiwango walichoonyesha kinathibitisha kuwa Misri inaweza kushindana na timu yoyote duniani licha ya kutokuwa na idadi kubwa ya wachezaji wanaocheza katika ligi kubwa za Ulaya.




