Mbappe ang’ara, Deschamps akoshwa

FOX BOROUGH: Nahodha wa Ufaransa, Kylian Mbappe, alifidia kukosa mkwaju wa penalti kwa kufunga bao la kuvutia lililoiongoza timu yake kuichapa Morocco mabao 2-0 na kutinga nusu fainali ya Kombe la Dunia 2026.
Katika mchezo wa robo fainali uliochezwa usiku wa Julai 9 mjini Foxborough, Massachusetts, Marekani, Mbappe aliifungia Ufaransa bao la kwanza dakika ya 60 kwa shuti la kupinda kutoka nje kidogo ya eneo la hatari, kabla ya Ousmane Dembele kuongeza la pili dakika sita baadaye na kuzima matumaini ya Morocco.
Kwa ushindi huo, Ufaransa sasa itakutana na mshindi wa robo fainali kati ya Ubelgiji na Hispania katika hatua ya nusu fainali.
Licha ya kukosa penalti dakika ya 28 baada ya kipa Yassine Bounou kuokoa mpira wake, Mbappe alionesha ubora wake kwa kufunga bao lake la nane kwenye michuano hiyo na kufikia mabao 20 katika historia ya Kombe la Dunia. Pia aliweka rekodi ya kucheza mechi 20 za Kombe la Dunia akiwa na umri wa miaka 27, akilingana na rekodi ya Wafaransa iliyokuwa ikishikiliwa na Hugo Lloris.
Kocha wa Ufaransa, Didier Deschamps, amesema ameridhishwa na hatua ambayo timu yake imefikia.
“Kufika nusu fainali mara tatu mfululizo ni jambo zuri. Inaonekana ni la kawaida, lakini lazima ufanye kazi kubwa kulifikia. Tuko pale tulipotaka kuwa,” amesema Deschamps.
Morocco, iliyokuwa ikisaka kucheza nusu fainali kwa mara ya pili mfululizo, ilishindwa kuonesha makali yake, huku ikimkosa mshambuliaji Ismael Saibari aliyekuwa majeruhi. Timu hiyo ilipiga shuti lake la kwanza lililolenga lango dakika ya 84.
Kocha wa Morocco, Mohamed Ouahbi, alikiri ubora wa wapinzani wao.
“Tumesikitishwa kwa kushindwa kufuzu. Ufaransa ni timu kubwa yenye wachezaji bora na walitengeneza nafasi nyingi zaidi. Leo walikuwa bora kuliko sisi, lakini tunaamini tutaendelea kukua na huenda tukawalipa kisasi baada ya miaka minne,” amesema.
Baada ya mchezo, Mbappe alisema safari yao bado haijaisha.
“Bado kuna kazi kubwa mbele yetu. Tunapaswa kuendelea kupambana kwa sababu hatua zinazofuata zitakuwa ngumu zaidi,” amesema mshambuliaji huyo wa Real Madrid.




