Chabada kusaka mabingwa wa baiskeli Dar

DAR ES SALAAM: CHAMA cha Baiskeli mkoa wa Dar es Salaam (CHABADA) kimeandaa mashindano ya mkoa Agosti 30 mwaka huu, ikiwa ni hatua ya kutafuta mabingwa watakaowakilisha katika mashindano ya Taifa yatakayofanyika Dodoma Septemba 12 na 13.
Mashindano hayo yanatarajiwa kuwakutanisha waendesha baiskeli kutoka wilaya zote tano za Dar es Salaam, huku chama hicho kikisema ushindani huo ni muhimu katika kuibua na kuandaa wachezaji watakaoiwakilisha Dar es Salaam kwenye mashindano ya taifa.

Akizungumza na SpotiLeo Mwenyekiti wa Chabada, Husseni Ali, amesema kwa muda mrefu mkoa huo haujaandaa mashindano ya kupata bingwa wa mkoa, hivyo wameamua kuyarejesha ili kutoa nafasi kwa waendesha baiskeli kujipima uwezo.
“Tumekaa vikao na kuona ni muhimu wachezaji washiriki mashindano haya kwa sababu kuna mashindano ya Taifa yatakayofanyika Septemba 12 na 13. Hatuwezi kupeleka mshindani kwenye timu ya taifa bila kufanya mashindano ya mkoa yatakayotupatia wawakilishi bora,” amesema.
Amesema waendesha baiskeli wanaume watashindana katika umbali wa kilomita 69, wakati wanawake watashindana kilometa 50.
Ali amewataka waendesha baiskeli wote wa Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi na kutumia mashindano hayo kama fursa ya kujenga historia na kuwania nafasi ya kuiwakilisha mkoa katika mashindano ya taifa.




