Ligi Kuu

Yanga yamtakia Kheri Miloud

DAR ES SALAAM: UONGOZI wa Klabu ya Yanga umetoa salamu za pongezi na kumtakia kheri aliyekuwa Kocha Mkuu wao, Hamdi Miloud, ambaye sasa ametambulishwa rasmi kuwa Kocha Mkuu wa Ismaily SC ya nchini Misri. Miloud amesaini mkataba wa mwaka mmoja na chaguo la kuongezewa mwaka mwingine kutegemeana na mafanikio.

Miloud anaondoka Yanga akiwa amevunja rekodi kwa kuiongoza klabu hiyo kutwaa mataji matatu muhimu katika msimu wa 2024/25. Mataji hayo ni ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Kombe la Shirikisho la CRDB na Kombe la Muungano mafanikio yaliyomfanya kuwa kwenye rada ya vilabu mbalimbali barani Afrika na kwingineko.

Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa Yanga, Ali Kamwe kuwa kocha Miloud alikuwa na mkataba wa muda mfupi wa miezi sita ambao umemalizika mara baada ya msimu kufungwa.

Ameongeza kuwa klabu ilikuwa katika hatua za awali za kufanya maboresho ndani ya timu, ikiwemo kujadiliana kuhusu benchi la ufundi, wakati ofa hiyo kutoka Misri ilipowasili.

“Miloud ni kocha mwenye rekodi nzuri na mafanikio ndani ya muda mfupi. Ni jambo la kawaida kwa klabu nyingine kumtazama kwa karibu. Kama uongozi, tulikuwa tayari kuendelea naye lakini mahitaji yake na mipango yake binafsi imepelekea kuchukua nafasi hiyo mpya,” amesema Kamwe.

Yanga SC imemaliza kwa kumtakia kila la kheri kocha huyo katika majukumu yake mapya, huku wakisema mafanikio yake ndani ya Jangwani yataendelea kukumbukwa na mashabiki wa timu hiyo.Kocha huyo sasa anatarajia kuanza safari mpya katika Ligi Kuu ya Misri.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button