Netflix yafanya mabadiliko ya filamu, vipindi

JUKWAA la kimataifa la kutazama filamu na vipindi mtandaoni, Netflix, limeanza mwezi Septemba kwa kufanya mabadiliko makubwa katika maktaba yake ya maudhui, huku filamu na vipindi kadhaa maarufu vikiondolewa kwenye huduma hiyo katika vipindi tofauti vya mwezi.
Miongoni mwa maudhui yanayoondolewa ni filamu maarufu za Rocky pamoja na mkusanyiko wa kazi tatu zinazohusiana (trilojia) ya Creed, huku baadhi ya vipindi na filamu nyingine zinazopendwa na watazamaji nazo zikiondolewa kulingana na ratiba ya Netflix.
Kwa mujibu wa ratiba ya maudhui inayotolewa kwa mwezi huu, baadhi ya filamu zilianza kuondolewa kuanzia Septemba 1, wakati vipindi vingine vimepangiwa kuondolewa katika siku zinazofuata.
Miongoni mwa vipindi vilivyopangiwa kuondolewa baadaye mwezi huu ni Girlfriends na Nashville, jambo linalowafanya mashabiki wa vipindi hivyo kuwa na muda maalumu wa kuvifuatilia kabla havijaondoka kwenye jukwaa hilo.Hata hivyo, Netflix haijaishia kwenye kuondoa maudhui pekee, bali pia imeandaa filamu, vipindi na maudhui mapya kwa ajili ya watazamaji wake katika mwezi huu.
Miongoni mwa maudhui yanayotarajiwa kuvutia hisia za watazamaji ni msimu mpya wa The Gentlemen, pamoja na Monster: The Lizzie Borden Story na Stranger Things: Tales From ’85.
Mabadiliko hayo ni sehemu ya utaratibu wa kawaida wa Netflix wa kusasisha maktaba yake, ambapo baadhi ya maudhui huondolewa baada ya muda wa leseni kumalizika na nafasi yake kuchukuliwa na maudhui mapya.




