Mastaa

Muhogo Mchungu: Wasanii waombe ridhaa kabla ya kutaja majina ya watu

DAR ES SALAAM: MSANII mkongwe wa filamu nchini, Abdalah Mkumbila Muhogo Mchungu, amesema ni muhimu kwa wasanii kuomba ridhaa kabla ya kutumia majina ya watu wengine katika kazi zao za kisanii ili kuepusha sintofahamu na kulinda heshima ya wahusika.

Muhogo Mchungu ametoa kauli hiyo akieleza kuwa baadhi ya wasanii wamekuwa na tabia ya kuwataja wenzao kwenye nyimbo bila kuwashirikisha au kuwaomba ruhusa kabla ya kurekodi kazi hizo.

Amesema utaratibu mzuri ni kwa msanii anayetarajia kutumia jina la mtu mwingine kwenye wimbo wake kuwasiliana naye kwanza kabla ya kuingia studio.

“Ni vyema wasanii wakaheshimiana. Kama unataka kulitumia jina la mtu kwenye kazi yako, ni vizuri ukamjulisha mapema na kupata ridhaa yake,” amesema.

Ametoa mfano, Muhogo Mchungu amesema msanii wa Bongo Fleva, Naseeb Abdul maarufu kama Diamond Platnumz, amewahi kumtaja katika moja ya nyimbo zake bila ya kumshirikisha jambo ambalo, kwa mtazamo wake, halikuwa sahihi.

“Hata mwanangu Diamond, alivyotaja jina la Muhogo Mchungu kwenye wimbo wake bila kuniambia, sidhani kama ilikuwa sahihi. Ilibidi aniambie kwanza kwa sababu huwezi kumtaja mtu bila ridhaa yake,” amesema.

Mbali na hilo, Muhogo Mchungu pia alidai kuwa hakulipwa stahiki zake baada ya kushiriki katika video ya wimbo wa Bush Party wa kundi la Solid Ground Family.

Kwa mujibu wa muigizaji huyo, alishiriki katika utengenezaji wa video hiyo kwa matarajio ya kupata malipo yake, lakini hadi sasa hajawahi kupokea fedha alizoahidiwa.

Kauli za Muhogo Mchungu zimeibua mjadala kuhusu umuhimu wa kuheshimu haki, mawasiliano na makubaliano kati ya wasanii wanaposhirikiana katika kazi mbalimbali za sanaa na burudani.

Wadau wa sanaa wanaamini kuwa kuwepo kwa maelewano na ridhaa kati ya wahusika kunasaidia kuimarisha ushirikiano na kuondoa migogoro isiyo ya lazima ndani ya tasnia ya burudani.

Related Articles

Back to top button