Kuelekea Valentine, Diamond aonesha Saa ya Sh Bilioni 1.2

DAR ES SALAAM: MSANII nyota wa muziki wa Bongo Fleva na Mkurugenzi Mtendaji wa Wasafi Media, Diamond Platnumz, anajiandaa kuachia wimbo wake mpya wa kimahaba uitwao ‘Natulizana’ ikiwa ni maalumu kwa msimu wa Valentine.
Hata hivyo, mbali na mashabiki kusubiri kwa hamu kazi hiyo mpya, gumzo kubwa limeibuka kuhusu saa ya kifahari inayoonekana kwenye video ya wimbo huo ikiwa na thamani ya Sh 60 milioni (sawa na TSh1.2 bilioni).
Katika kikao cha maandalizi ya video hiyo pamoja na timu yake ya uzalishaji akiwemo kaka yake Romy Jons, Diamond alidokeza kuhusu uwepo wa saa hiyo ya bei mbaya itakayopamba picha za video.
“Kuna kidonda kimoja cha 1.2B hapo kimeoneshwa,” aliandika Diamond kupitia ukurasa wake wa Instagram huku akiitambulisha timu ya watayarishaji wa video hiyo, jambo lililozua mjadala mkali mitandaoni.
Diamond si mgeni katika kuonesha maisha ya kifahari. Mwaka jana pekee, alionekana akiwa amevalia mavazi ya wabunifu wa kimataifa yenye thamani ya dola 265,000.
Katika mahojiano ya mwaka 2016, msanii huyo alikadiria utajiri wake kufikia Sh516 milioni (takribani dola milioni 4), na kufikia mwaka 2018 alihamia katika jumba lake la kifahari lenye thamani ya Sh99 milioni lililopo Mbezi Beach, Dar es Salaam.
Magari ya Kifahari na Usafiri wa Hadhi ya Juu
Ukichunguza zaidi maisha ya Diamond, utagundua mkusanyiko mkubwa wa magari ya kifahari unaoongozwa na Rolls-Royce Cullinan ya mwaka 2021 pamoja na Cadillac Escalade kadhaa zilizoboreshwa maalum.
Ripoti pia zinaeleza kuwa msanii huyo ana uwezo wa kutumia ndege binafsi, ishara ya hadhi ya juu katika usafiri wa watu matajiri duniani.
Mbali na magari, Diamond pia anafahamika kwa mapenzi yake ya vito na vifaa vya thamani, ikiwemo saa aina ya Richard Mille RM 011 na grillz za meno zilizopambwa kwa almasi zinazodaiwa kugharimu zaidi ya Sh5.2 milioni.
Wakati mashabiki wakisubiri kuiona video ya “Natulizana”, ni wazi kuwa mbali na muziki, mitindo na maisha ya kifahari ya Diamond Platnumz yataendelea kuwa gumzo kubwa ndani na nje ya Tanzania.




