Mashujaa FC wanashusha Vyuma tu!

KIGOMA: Wazee wa mapigo na mwendo Mshajaa FC kutoka mkoani Kigoma umekamilisha usajili wa kiungo kutoka Geita Gold FC, Yusuph Dunia kuitumikia kikosi cha timu hiyo kwa msimu wa 2024/25 wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Dunia ni mchezaji wa pili kusajiliwa ndani ya kikosi hicho baada ya kufanikiwa kumnasa kiungo mwingine, Ally Nassoro ‘Ufudu’ akitokea Kagera Sugar.
Kocha Mkuu wa Mashujaa FC, Mohammed Abdallah ‘Bares’, amesema wanafanya maboresho ya kikosi kulingana na mahitaji yake kwa msimu ujao kwa kuangalia kila eneo lililopo na mapungufu.
Amesema wamefanikiwa kupata huduma ya nyota wawili na uongozi unaendelea na mchakato wa kusajili kupita mapendekezo ya ripoti aliyokabidhi kuimarisha kikosi katika kila eneo.
“Ripoti inaeleza madhaifu ya msimu uliopita na sasa tunaboresha kila eneo ili kujenga timu imara na kutorudia makosa yaliyopita, bado tunaendelea kusajili kwa sababu kuna safu ya ulinzi na kuboresha ushambuliaji,” amesema Bares.
Amesema kuna makosa yatayojirudia katika usajili, anaimani na viongozi kufuata maagizo aliyowapa kwenye ripoti na tathimini ya timu yao kwa msimu uliopita ambao walicheza kwa presha kubwa ya kutoshuka daraja.